Mkuu wa mkoa wa Mtwara Mhe. Gelasius Byakanwa akisalimiana na wanafunzi wa shule ya Sekondari Aquinas alipowasili shuleni hapo katika hafla fupi ya kupongezana mara baada ya matokeo ya kidato cha sita 2018 ambapo mkoa wa Mtwara uliongoza kitaifa
Methali moja ya kihaya inasema ‘Abachumita Empunu Bema Lubaju Lumo’. Tafsiri ya kiswahili ni kwamba
wachomao mkuki nguruwe pori, hukaa upande mmoja. Methali za Kiswahili
zinazofanana na msemo huu ni umoja ni nguvu utengano ni udhaifu. Kichango
huchangizana. Wafanyao kazi inayofanana, hunia mamoja.
Methali hii inatafakari kubwa katika njia tuliyoianza kama
mkoa. Tumepiga hatua ndefu ya mapambano dhidi ya adui ujinga. Hatua hii ndiyo
imetufikisha katika nafasi ya nane kati ya mikoa 26 katika matokeo ya darasa la
saba 2018 kutoka nafasi ya 22 mwaka 2017.
Takwimu za nyuma si njema sana kwa mkoa kwani mwaka 2015 mkoa
ulishika nafasi ya 12 wakati Mwaka 2016 ulishika nafasi ya 25.
Mafanikio haya huwezi kuyatenganisha na matokeo ya kidato cha
sita 2018 ambapo mkoa umekuwa wa kwanza katika mikoa yote ya Tanzania bara na
visiwani.
Tunaweza kuainisha sababu nyingi za ufaulu lakini hatutaacha kusema
umoja na mshikamano kati ya viongozi na wadau wa Elimu mkoani Mtwara umechangia
kwa kiasi kikubwa mafanikio haya.
Umoja huu ndio unatoa nafasi ya pongezi nyingi kwa Mkuu wa
Mkoa wa Mtwara Mheshimiwa Gelasius Byakanwa Kwa jitihada zake tangu alipopewa
nafasi ya kuongoza mkoa huu Oktoba 26 mwaka jana.
Jitihada hizi zilianza kuonekana tangia vikao vyake vya awali
na wadau wa Elimu ikiwemo kikao maalumu cha kamati ya Ushauri ya Mkoa
kilichotoka na mikakati mbalimbali aliyoahidi kuisimamia.
Jitihada hizi ni pamoja na zile zilizobainisha shule 10 ndani
ya halmashauri ya Wilaya ya Mtwara ambazo wanafunzi wake walikuwa wakisomea
kwenye mikorosho. Wadau kwa pamoja wakamuunga mkono kwa michango mbalimbali
hatimaye leo hii watoto wanasomea kwenye madarasa mazuri ya kisasa.
Jitihada hizi ndizo zilizoagiza wanafunzi na walimu wote
wanaoacha alama ya mafanikio shuleni kwao kutambuliwa kwa utaratibu maalumu wa
vibao wa wazi kama motisha kwa wengine. Ni jitihada hizihizi zilizoagiza walimu
kumaliza mtaala mapema mwezi Juni ili kuwapa muda wanafunzi kufanya majaribio na
marudio.
Kwa mikakati hii nakubaliana na baadhi ya wadau walioandika
sehemu mbalimbali kukubaliana na mikakati ya mkoa akiwemo aliyewahi kuwa Waziri
wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
na Mbunge wa Jimbo la Mtwara vijijini Mheshimiwa Hawa Ghasia ambaye aliandika
kwenye kundi la whatsap la viongozi wa mkoa. (Mtwara Leaders Group)
“Napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mkuu wa Mkoa Mheshimiwa Byakanwa, viongozi na watendaji wa ngazi zote kwa kuwezesha mkoa wa Mtwara kushika nafasi ya Nane kitaifa. Ushirikiano, mshikamano na usimamizi madhubuti chini ya uongozi wako matunda tumeanza kuyaona haraka kuliko tulivyotarajia”
Mkuu wa Mkoa Mhe. Gelasius Byakanwa akishiriki ujenzi wa shule ya Msingi Mitambo. Hii ni moja kati ya shule kumi ambazo wanafunzi wake walikuwa wakisomea chini ya Mikorosho.
Inawezekana kabisa alikosekana wa kutukalisha Lubaju lumo
(upande mmoja) dhidi ya mila na tamaduni zinazokwamisha elimu kwa mikoa ya kusini.
Inawezekana alikosekana wa kutukalisha lubaju lumo katika mapambano
dhidi ya mimba shuleni.
Inawezekana tulishindwa kuwa pamoja katika kuwasimamia walimu
kutimiza wajibu wao. inawezekana tulishindwa kuwa lubaju lumo katika
kumuwezesha mtoto afahamu nia njema ya mzazi kumpeleka shule.
Hisia hizi zinakumbusha moja ya maneno ya Naibu Waziri wa
Elimu, Sayansi Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi Mhe. William Ole Nasha wakati
akizungumza na viongozi wa Mkoa pamoja na Wakuu wa shule za sekondari za kidato
cha sita mkoani Mtwara katika ukumbi wa shule ya sekondari ya ufundi Mtwara
mara baada ya matokeo ya kidato cha sita kitaifa 2018. Mheshimiwa Nasha
alisema.
“Hakuna kinachoitwa
kufaulu kwa coincidence. Haitokei bahati mbaya. Panapoufaulu kuna jitihada,
kuna uongozi, kuna watu wamefanya kazi. Ndiyo maana nafurahi kuja kukutana na
ninyi viongozi wa mkoa na wakuu wa shule za sekondari za kidato cha sita mkoa
wa Mtwara kuwaambia mmefanya kazi nzuri.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi Mhe. William Ole Nasha akizungumza na wanafunzi wa shule ya sekondari ya Ufundi Mtwara. (hawapo pichani)
Huu ndio ukweli usiopingika kwamba viongozi na wadau wote wa
elimu wameshikamana, wakaandaa
mazingira, wakasimamia, hatimaye Mkoa umeiona njia waliyoitafuta kwa muda mrefu.
Bila mshikamano wa viongozi na wadau wote wa elimu, hata kama
kuna fursa nzuri ya kusoma matokeo chanya hayatapatikana. ndiyo maana katika
moja ya wimbo wa hayati Bob Marley, ‘Get up Stand up’ anasema.
‘In the Abundant of
water, the fool is thirsty’. tafsiri ya Kiswahili isiyo rasmi ni kwamba ‘Katikati ya maji mengi, mpumbavu analia kiu’.
Maneno haya ya Bob Marley ukiyahusianisha na Maneno ya Mheshimiwa
Nasha utatambua kwamba wapumbavu hawa anaowataja Bob Marley wanaweza kuwa
wameshindwa kuyapata maji kwa sababu ya kukosa uongozi. inawezekana maji haya
yako sentimeta tatu ardhini, mhandisi wa maji hajawasaidia. inawezekana maji
haya yamefunikwa na majani. inawezekana maji haya yamejazwa kwenye chungu
kilichofunikwa, Inawezekana maji haya yanapatikana kwenye miti ya aina fulani. Bila
wataalamu na viongozi wao kuwasaidia wataendelea kulia kiu.
Uongozi unahusika katika mafanikio ya jambo lolote.
Sasa
tumeianza safari ya mafanikio mkoani Mtwara. Tunapongezana viongozi wote wa
mkoa wa Mtwara kwamba tumeweza. Wakati tukifurahia hatua tuliyoifikia tukumbuke
maneno ya Mhe. Mkuu wa Mkoa wakati wa hafla fupi ya kupongezana baada ya matokeo
ya kidato cha sita 2018 pale ukumbi wa shule ya sekondari Aquinas.
“Ndugu zangu inaweza isiwe wakati mzuri
sana wa kubweteka kwamba tumefanya vizuri. Kuna wasiopenda kuiona Mtwara ikiwa
katika nafasi hiyo. hawa watakua na mikakati, watakuwa na mipango, watakuwa na
mbinu za kuhakikisha kesho wanaiona Mtwara ikisomeka kumi naa au ishirini”.
Hongereni,
Viongozi wa Mkoa wa Mtwara. Mmethubutu na Mmeweza. Mzidi kusonga mbele.
No comments:
Post a Comment