Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa Mheshimiwa Balozi Dkt. Augustine
Phillip Mahiga amesema moja ya uwekezaji unaotarajiwa kufanywa na
wajerumani hapa nchini ni ujenzi wa kiwanda cha Mbolea mjini Mtwara.
Mheshimiwa Mahiga ameyasema hayo juzi mara baada ya kikao kifupi na
Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Ujerumani Mhe. Heiko Maas aliyekuwa
katika ziara ya siku mbili hapa nchini. Amesema kiwanda hicho kitakuwa
kikubwa kuliko vyote Afrika.
‘Tumezungumzia eneo la uwekezaji,
uwekezaji katika sekta mbalimbali za viwanda. viwanda katika kutengeneza
ajira, viwanda kutuwezesha sisi kufikia lengo letu la kufikia uchumi wa
kati ifikapo 2025 na Ujerumani kama nchi yenye nguvu, na ambayo ina
uwezo mkubwa kuliko nchi zote za magharibi mwa Ulaya inaweza kuwa
Mwekezaji mkubwa katika nchi yetu.
Tayari sasa hivi tunazungumza uwekezaji
wa kiwanda ambacho kitakuwa kikubwa kuliko vyote Afrika, kiwanda cha
kutengeneza mbolea huko Mtwara. kiwanda ambacho kitasaidia wakulima na
kitatengeneza ajira kwa watanzania’ Amesema Balozi Mahiga.
Mheshimiwa Mahiga ambaye anaongoza
Wizara ambayo inadhamana ya kujenga mahusiano mazuri kati ya Tanzania na
Nchi za Nje amesema uhusiano wa Tanzania na Ujerumani ni wa kihistoria
na ndiyo maana Waziri huyo ambaye amepewa nafasi hiyo hivi majuzi
ameamua kufanya ziara yake ya kwanza Barani Afrika hapa nchini.
Amesisitiza kuwa kutokana na uwezo mkubwa wa uchumi wa taifa la
Ujerumani wanauwezo wa kuwa wawekezaji wakubwa katika nchi yetu.
Majadiliano ya ujenzi wa kiwanda cha mbolea kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya HELM yenye makao yake Ujerumani yalianza miaka kadhaa huko nyuma. Hati ya Makubaliano (Memorandum of Understanding) kati ya Kampuni hiyo na Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Mtwara (RCC) kwa niaba ya Wananchi wa Mkoa wa Mtwara ilisainiwa Julai 21, 2014.
Matarajio makubwa ya wananchi wa Mtwara
ni kuwa kujengwa kwa kiwanda hiki kutawezesha ndoto ya uongozi wa Mkoa
wa Mtwara kuhakikisha ifikapo mwaka 2035 Mtwara kinakuwa kituo muhimu
cha uwekezaji na kitovu cha huduma na shughuli muhimu za usafiri na
usafirishaji katika ukanda wa mikoa ya kusini mwa Tanzania hususani
mikoa ya Lindi, Mtwara Ruvuma na Njombe na ukanda wa maendeleo wa Mtwara
ambao unahusisha nchi za Tanzania, Msumbiji, Malawi, Zambia na Afrika
ya kusini.
Pia kuifanya Mtwara kuwa Jiji lenye
ustawi wa maisha shindani na majiji yaliyo kwenye ukanda wa bahari ya
hindi, mashariki na kusini mwa Afrika.
No comments:
Post a Comment