MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Thursday 17 May 2018

Wadau wapongeza mikakati ya kuboresha elimu mkoani Mtwara

Mpango wa kuhamasisha elimu mkoani Mtwara kwa kuwatambua walimu na wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo umepongezwa na wadau wa Elimu hapa nchini. Mpango huo ulioanzishwa Na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mheshimiwa Gelasius Byakanwa unahusisha kuweka vibao vya kumbukumbu ya majina ya Walimu na wanafunzi waliofanya vizuri kwa kila mwaka.

Akizungumza mara baada ya ziara ya kutembelea maeneo yanayotekeleza mradi wa Tusome pamoja mkoani Mtwara, iliyofanywa na wadau wa mradi huo kutoka mikoa inayoutekeleza hapa nchini, Mshauri wa Elimu mkoa wa Lindi kupitia shirika lisilo la kiserikali la ‘Education Quality Improvement Program’ (EQUIP-T) Digner Peter amesema mpango huo ni mzuri na unatoa hamasa kwa wanafunzi na walimu kufanya jitihada zaidi.
Digner Peter
“Kilichonifurahisha sana ni vile vibao nilivyoviona hapo shule ya Msingi Mihambwe. Niliona vibao ambavyo vinamtangaza mwalimu bora na mwanafunzi bora... Sisi tunaweza kuwa tunakiona kama ni kitu kidogo, Jamani hicho siyo kitu kidogo kwa wenzetu wazungu wangekikuza hicho. Mtu kuacha historia nzuri mahari siyo kitu kidogo. Hata kwa hela zangu nitatafuta shule hata moja Nikakifanye”. Ameeleza Digner.
  
Kuhusu msaada unaotolewa na Mradi wa Tusome pamoja katika kuinua elimu mkoani Mtwara Mwalimu Siwema Mrope wa Shule ya Msingi Mbuo Wilayani Mtwara ameshukuru kwamba hali hiyo imewajengea hamasa watoto kujifunza na kuwaamusha wazazi kujitolea kuchangia mambo mbalimbali katika elimu.

Siwema Mrope
 Amesema yeye binafsi alipatiwa mafunzo ya kufundisha watoto wadogo. Amesema kabla ya mradi wa tusome pamoja kutekelezwa katika shule yake, elimu ya awali haikuwa ikipewa kipaumbele. Wazazi na watu mbalimbali katika jamii walikuwa wakiiona kama vile haina umuhimu. Baada ya kuingia kwa mradi huu watu wote wametambua na wanatoa ushirikiano wa hali ya juu.

Ameitaka Serikali ihakikishe inawekeza zaidi katika hatua ya mwanzo ya elimu ya watoto kwani hata maprofesa walijengwa katika hatua ya awali.

Fatuma Mode Ramadhani
Fatuma Mode Ramadhani. Afisa Elimu Maandalizi Zanzibar amesema amefurahishwa na jinsi ambavyo walimu walivyo na moyo wa kufundisha mkoani Mtwara. Anasema hali hiyo inaweza isiwe ngeni katika maeneo mengi lakini hiyo ndiyo njia bora ambayo Taifa linaweza kupiga hatua.

“Lazima kuwepo ushirikiano wa makundi yote hayo katika jamii”. Alisisitiza.

Amina Abdallah
Kwa upande wake Amina Abdallah Nanyamo wa kijiji cha Mbuo wilayani Mtwara anasema kabla ya ujio wa Mradi wa Tusome Pamoja watoto walikuwa wakiogopa kwenda shule kwa kile walichosema ukienda shule utabadili dini kutoka Uislam na kuwa Mkristo, lakini utaratibu wa Tusome pamoja ambao ulikuja na kuboresha miundombinu ya shule na kuwashirikisha wazazi katika malezi ya watoto shuleni, ulifanya jamii ibadilike na kuanza kutambua kuwa shule inatoa maadili na misingi ya maisha ya baadaye, wala siyo kumbadili mtoto dini. 
Rehema Ibrahim
Rehema Ibrahimu ambaye ni Mhamasishaji Jamii wa shule ya Msingi Mbuo yeye alisema Mradi wa Tusome Pamoja umeifanya jamii itambue kwamba shule ni mali yao si mali ya walimu. Jambo lililobaki Tusome pamoja watuwezeshe na sisi twende tukajifunze kwa wenzetu. 


kwa upande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Mtwara Alfred Luanda amewakumbusha wadau wote wa Elimu kuhakikisha wanazingatia maadili ya elimu. Amesema Taifa bora litajengwa kwa kuweka misingi imara katika elimu. Ametaja moja ya changamoto ambazo zinaikumba elimu kuwa ni pamoja na matumizi ya vitabu hasa pale shule zinapotofautiana katika aina ya vitabu vinavyotumika kufundishia watoto.

Alfred Luanda
Ameusifu mradi wa Tusome Pamoja kwamba ni mzuri na unachangia kwa kiasi kikubwa katika maendeleo ya Taifa kwani Taifa lolote linalotamba duniani liliwekeza katika elimu. “Hata maandiko matakatifu yanasisitiza elimu”. Amesema Luanda.


Katika ziara hiyo iliyofanywa katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara na Tandahimba mkoani Mtwara iliwahusisha wadau kutoka mikoa ya Lindi, Mtwara, Morogoro, Iringa na Zanzibar kwa lengo la kujifunza jinsi Mradi wa Tusome pamoja unaodhaminiwa na Watu wa Marekeni unavyotekelezwa mkoani Mtwara.

Mradi huo umesaidia maeneo mbalimbali ikiwemo mafunzo kwa walimu jinsi ya kufundisha watoto wa awali na wale wa darasa la kwanza na la pili. Aidha mradi huu umeenda mbali kwa kuweka miundombinu ya kujifunza na kufundishia katika shule mbalimbali.


No comments:

Post a Comment