MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Friday 22 March 2019

ISHI KWA KUFUATA MTINDO BORA WA MAISHA ILI UEPUKE MAGONJWA SUGU YASIYO YA KUAMBUKIZA

ISHI KWA KUFUATA MTINDO BORA WA MAISHA ILI UEPUKE  MAGONJWA SUGU YASIYO YA KUAMBUKIZA


Na; Herieth Joseph Kipuyo, Evaristy Masuha
Magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza ni kisukari, magonjwa ya moyo, shinikizo kubwa la damu, magonjwa ya figo, saratani na magonjwa sugu kwa njia ya hewa. 

Kwa Mujibu wa takwimu za Afya Mkoa wa Mtwara (DHIS2, 2018) watu 34,667 Mkoani Mtwara wameathirika na kisukari, magonjwa ya moyo na shinikizo kubwa la damu. 

Ukiacha takwimu hizi, Kidunia magonjwa ya saratani, kisukari, matatizo ya kupumua na maradhi ya moyo  husababisha vifo vya watu milioni14 kwa mwaka ikiwa ni asilimia 71 ya  vifo vyote duniani. Idadi hiyo inajumuisha watu milioni 15 ambao hupoteza maisha mapema kati ya umri wa miaka 30 na 70 kutokana na magonjwa sugu yasiyo ya kuambukiza. Hii ni kwa mjibu wa taarifa ya Shirika la Afya Duniani (WHO, 2018).

Kutokana na ukubwa wa tatizo hili Afisa Habari Mkoa wa Mtwara, Evaristy Masuha akishirikiana na Afisa Lishe Mkoa, Herieth Joseph Kipuyo watakuwa wakikuletea mwendelezo wa makala mbalimbali zinazoelezea njia za kujikinga na maradhi haya sambamba na ulaji unaoshauriwa kwa mtu aliye athirika na magonjwa tajwa. Makala hizi zitakuwa zikirushwa kila jumamosi kwenye makundi mbalimblai ya kijamii, tovuti ya Mkoa wa Mtwara www.mtwara.go.tz, mtwarars.blogspot.com, facebook page ya Mtwarars magazeti pamoja na vyombo mbalimbali vya habari.

MTINDO BORA WA MAISHA:
Mtindo bora wa maisha ni ule unaozingatia ulaji unaofaa, kuepuka matumizi ya pombe, kuepuka uvutaji wa sigara na bidhaa zinazotokana na tumbaku, kuepuka msongo wa mawazo na kufanya mazoezi ya mwili.

1.  ULAJI UNAOFAA:
Epuka vyakula na vinywaji vyenye sukari kwa wingi. Pendelea kutumia matunda au juisi halisi ya matunda na mbogamboga kwa wingi. Vyakula vyenye sukari kwa wingi husababisha uzito mkubwa wa mwili ambao ni miongoni mwa sababu za magonjwa tajwa hapo juu.

Epuka vyakula vyenye wingi wa mafuta. Tumia mafuta kidogo wakati wa kupika na pendelea zaidi mapishi yasiyotumia mafuta mengi kama kuoka, kuchemsha, kuchoma, mvuke, kutokosa n.k. Halikadhalika epuka vyakula vyenye lehemu (cholesterol) kwa wingi kama nyama nyekundu ya nguruwe, ng'ombe, mbuzi n.k. Endapo itatumika mtu mmoja asizidishe nusu kilo kwa wiki. Pendelea zaidi samaki,  nyama ya kuku na vyakula jamii ya kunde (nyama ya kuku ondoa ngozi). Tumia mafuta ya asili ya mimea mfano karanga, korosho, alizeti, ufuta, nazi  n.k.

Epuka vyakula vilivyopita muda wa matumizi au vyakula vilivyoharibika/kuoza mfano mahindi, karanga n.k. kwani huwa na sumu kuvu ambayo huusababisha saratani ya ini.
Epuka matumizi ya chumvi kwa wingi. Matumizi ya chumvi kwa mtu mmoja kwa siku ni gramu 5 (kijiko kidogo cha chai). Chumvi ikizidi huweza kusababisha tatizo la shinikizo kubwa la damu na baadhi ya saratani kama ya utumbo. Tumia viungo kuongeza ladha ya chakula badala ya kutumia chumvi kupita kiasi. Viuongo hivyo ni kama vitunguu saumu, tangawizi n.k.
Kula mbogamboga na matunda kwa wingi punguza wanga na protini
Epuka unene uliozidi/uliokithiri
Kunywa maji ya kutosha: Maji hayahesabiwi kama kundi la chakula lakini yana umuhimu mkubwa sana mwilini. Inapaswa kunywa maji safi na salama ya kutosha angalau glasi nane kwa siku au lita moja na nusu. Unaweza kuongeza maji mwilini kwa kunywa supu, madafu, togwa na juisi halisi za matunda mbalimbali. 
EPUKA MATUMIZI YA POMBE:
Pombe husababisha ongezeko la uzito mkubwa wa mwili linalohusishwa na magonjwa sugu yasiyo ya kuambukizwa. Kwa upande mwingine pombe hupunguza uwezekano wa ini kufanya kazi vizuri na hivyo kuathiri uwekaji wa akiba ya vitamini na madini mwilini.  Aidha, pombe inaongeza sana uwezekano wa kupata saratani ya koo, koromeo, mdomo, matiti n.k. 

(Gm 1 ya pombe ni sawa na kalori 7 hivyo bia moja ni sawa na kalori 840 ambapo ni sawa na mkate mdogo wa silesi).
EPUKA MATUMIZI YA SIGARA NA BIDHAA NYINGINE ZA TUMBAKU:  Sumu aina ya nikotini iliyopo katika sigara, huharibu ngozi ya ndani ya mishipa ya damu hivyo huongeza uwezekano wa lehemu (cholesterol) kujikusanya kwenye mishipa ya damu zilizoathiriwa na kusababisha magonjwa ya moyo. Nikotini pia huweza kusababisha mishipa ya damu kuziba au kuwa myembamba na hivyo kuzuia damu kupita inavyotakiwa. Halikadhalika sigara husababisha saratani ya mapafu, kinywa na koo.
 FANYA MAZOEZI YA MWILI :
Ni muhimu kwa binadamu wote, mtoto, mtu mzima mgonjwa au mwenye afya, mnene au mwembamba kufanya mazoezi kwani husaidia mifumo mbalimbali ya mwili kufanya kazi kwa ufanisi. Mazoezi huzuia ongezeko la uzito mkubwa wa mwili, hupunguza uwezekano wa kupata saratani, magonjwa ya moyo na shinikizo kubwa la damu. Fanya mazoezi ya mwili angalau dakika 30 kila siku na kutokwa jasho. Dumisha mazoezi ya mwili kwa kufanya shughuli mbalimbali za nyumbani, kutembea kwa miguu badala ya kutumia usafiri wakati wote, kupanda gorofa kwa ngazi badala ya kutumia lift n.k.
 EPUKA MSONGO WA MAWAZO:
KUMBUKA: unene uliozidi au kithiri ni miongoni mwa sababu inayochangia magonjwa ya kisukari, magonjwa ya moyo na shinikizo kubwa la damu. Wasiliana na wataalamu ili uweze kujua uzito unao takiwa kuwa nao kulingana na urefu wako

Tahadhari: Mama mjamzito haruhusiwi kupunguza uzito hadi atimize miezi sita (6) baada ya kujifungua.

Usikose makala ijayo ambayo itazungumzia ulaji kwa mgonjwa wa kisukari

Unaweza kupata ushauri au maelezo ya ziada kwa kupiga simu namba 0766269887/0658137610 - Ushauri bure



No comments:

Post a Comment