Mikoa ya Mtwara na Lindi sasa imeandika historia mpya baada ya kuzinduliwa kwa mitambo mipya miwili ya kuzalisha umeme yenye uwezo wa kuzalisha megawati nne na kufanya kituo cha Mtwara kuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 22 kutoka megawati 18.
Mitambo hiyo imewashwa leo na Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani saa 5:20 asubuhi katika
kituo cha Mtwara kinachohudumia mikoa ya Lindi na Mtwara. mitambo hiyo imegharimu
kiasi cha Sh bilioni 8.5 na hivyo kuongeza wigo mpana katika sekta ya uwekezaji
katika miradi inayohitaji umeme.
Akizungumza katika
hafla ya kuwasha mitambo hiyo, Dkt Medard Kalemani amesema kutokana na mikoa ya
Lindi na Mtwara kukuwa kiuchumi tayari wameanza utaratibu wa kuagiza mitambo mingine
miwili ili kufanya kituo cha Mtwara kuzalisha megawati 26 na kuwa na ziada ya
umeme lakini kuvutia zaidi wawekezaji hasa wanaohitaji umeme wa uhakika.
“Tulichokifanya leo, hizi mashine mbili mpya, tumeziingiza
sasa kwenye gridi ya taifa na kuongeza megawati Nne, na kufanya jumla ya
megawati 22 kwa mikoa ya Mtwara na Lindi. Kwa sasa mahitaji ya mikoa ya Lindi
na Mtwara ni takribani megawati 16.” Amesema Waziri.
Naye Mkuu wa Mkoa wa
Mtwara Mheshimiwa Gelasius Byakanwa ameishukuru serikali kwa jitihada
wanazoendelea nazo kuhakikisha tatizo la Umeme Mkoani Mtwara linaisha na kuwataka
wananchi wa Mkoa wa Mtwara kuwekeza katika shughuili mbalimbali za kiuchumi
ikiwemo viwanda vidogovidogo.
“Sasa umeme wa uhakika
upo, ningependa kuona wananchi wanautumia kuboresha maisha yao na hata kuwekeza
katika viwanda vidogo vidogo ili tuweze kufikia katika uchumi wa kati,”amesema
Byakanwa
Meneja wa mradi Mhandisi,
Mkulungwa Chinumba ameishukuru serikali kwa kuhakikisha inatatua changamoto za
uzalishaji wa nishati ya umeme mikoa ya kusini. Aidha ameahidi kuzitunza
mashine hizo kwa kuweka utaratibu mzuri ya matengenezo pale zinapoharibika.
Nao wabunge wa wa mkoa wa Mtwara akiwemo Mhe. Chikota wa
jimbo la Nanyamba na Mhe. Hawa Ghasia wa jimbo la Mtwara vijijini wameishukuru
serikali kwa kuwezesha kukamilika kwa mradi huo. Wamesema wananchi walikuwa
wakikwama kufanya kazi kutokana na kutokuwa na uhakika wa umeme hasa kipindi
ambacho mashine zilikuwa zimeharibika.
Wamesema msingi wa uchumi wa viwanda ni umeme hivyo wananchi
wa mikoa ya Kusini wanapaswa kuchangamkia fursa hii.
Akizungumzia manufaa ya huduma hiyo Yahaya Salumu mkazi wa
Mtwara mjini ameishukuru serikali. amesema msingi wa uchumi wa viwanda ni
uhakika wa umeme, aidha ameomba gharama za kuingiza umeme majumbani zipunguzwe
ili wananchi wengi wa hali ya chini wapate huduma hiyo.
No comments:
Post a Comment