MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Wednesday 23 May 2018

Muarobaini wa tatizo la Umeme Mtwara wapatikana



Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mhe. Gelasius Byakanwa mara baada ya kuuwasili Uwanja wa ndege wa Mtwara
 
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (MB) amezindua mradi wa umeme ambao utaunganisha mikoa ya Mtwara na Lindi katika Gridi ya Taifa. Kabla ya mradi huu Mikoa hii miwili ilikuwa ikipokea nishati hiyo kutoka kwenye kituo cha kuzalisha umeme kilichoko Mtwara mjini ambapo mahitaji ya Mikoa ya Lindi na Mtwara kwa sasa yamekuwa yakitajwa kuwa ni megawati 16.5.



Akizindua mradi huo katika kituo cha kuunganisha nishati hiyo kijijini Mahumbika Lindi Mheshimiwa Waziri Mkuu amesema kwamba mradi huo ni miongoni mwa ahadi ya serikali ya awamu ya tano ya kuhakikiisha inatatua changamoto zote zinazokwamisha maendeleo.

Amesema hiyo ni fursa muhimu kwa mikoa ya Lindi na Mtwara kualika wawekezaji hasa baada ya kuondokana na tatizo la nishati ya umeme.

Baada ya zoezi hilo lililofanyika huko Lindi Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyekuwa na ziara ya siku moja katika mikoa hii miwili amezindua upanuzi wa kituo cha kufua umeme kilichoko Mtwara mjini ambapo serikali ya awamu ya tano imeongeza mashine mbili zenye uwezo wa kufua megawati 2 kila moja. Hilo linakifanya kituo hicho kilichokuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 18 kuanza kuzalisha megawati 22.

Kwa miezi ya hivi karibuni mikoa ya Mtwara na Lindi ilikumbwa na changamoto kubwa ya kukatika katika kwa umeme hasa kutokana na kuharibika kwa baadhi ya mashine katika kituo hicho. Kufuatia hali hiyo serikali iliahidi kununua mashine mbili na kuzifanyia matengenezo mashine zilizoharibika. Ahadi hiyo imekamilika.
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majailiwa Majaliwa akishangilia pamoja na wanamtwara mara baada ya uzinduzi wa usafirishaji wa mafuta kupitia Bandari ya Mtwara

Baada ya zoezi la miundombinu ya Umeme Mheshimiwa Waziri  Mkuu amezindua usafirishaji wa mafuta kupitia Bandari ya Mtwara. Kabla ya hatua hii mkoa wa Mtwara na mikoa yote ya kusini ilikuwa ikipata mafuta kutokea Bandari ya Dar es Salaam hali ambayo ilikuwa ikiifanya nishati hiyo kuuzwa kwa bei ya juu kutokana na gharama za usafirishaji kutoka Dar es Salaam.

Akizungumzaia mafanikio ya hatua hiyo Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mheshimiwa Gelasius Byakanwa amesema mambo yote haya mawili yanatoa fursa ya mkoa kuchagamuka zaidi. Mafuta haya yanatarajiwa kuchukuliwa hapa mkoani na kusafirishawa ndani na nje ya nchi. Ametoa wito kwa wawekezaji kuja mkoani Mtwara kwani Fursa kubwa zimefunguka.

No comments:

Post a Comment