MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Wednesday 4 April 2018

Ufisadi wa kutisha korosho Mtwara. RC afyatuka awatumbua Kibao

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mhe. Gelasius Byakanwa ameagiza kuchukuliwa hatua za kisheria Meneja Wa Chama cha Ushirika cha Tandahimba na Newala (TANECU), Afisa Ushirika wilaya ya Tandahimba, Makatibu wa Vyama kadhaa vya msingi na baadhi ya wananchi ambao wameshiriki katika ufisadi wa kutisha katika kilimo cha korosho mkoani hapa.

Mheshimiwa Byakanwa amechukua uamuzi huo baada ya kupokea taarifa ya uchunguzi wa madai ya malipo ya fedha za wakulima wa korosho msimu wa mwaka 2016/20117 na 2017/2018 katika Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba ambayo iliundwa na Mkuu wa Wilaya hiyo Mheshimiwa Sebastian Muungano Walyuba. 

Amesema katika taarifa hiyo aliyoipokea wiki iliyopita Wilayani Tandahimba  imeonesha Meneja wa Chama Kikuu cha cha Ushirika cha Wilaya ya Tandahimba na Newala (TANECU) Mohamed Nassoro  alishiriki kufanya maamuzi kinyume na utaratibu hasa baada ya kubainika upotevu wa kilo 194,479 zilizokuwa zimehifadhiwa katika ghala lililokuwa chini ya MMZ Company LTD msimu wa 2017/2018. Anasema baada ya kubainika upotevu huo ambao haukuripotiwa katika chombo chochote cha ulinzi na usalama  viongozi wa TANECU chini ya Meneja huyo walikubaliana na ahadi ya mtunza ghala huyo kuwa atalipia upotevu huo kwa bei ya tsh 1,850 kwa kilo, ambapo thamani ya kilo zote ni  Tsh 359,786,150.

Amesema maamuzi hayo yanatia shaka hasa ikizingatiwa kuwa bei ya shilingi 1,850 waliyokubalina kulipa kwa kila kilo ilikuwa ni bei ya chini kabisa katika bei zote kwani korosho ziliuzwa hadi shilingi 4128. Aidha ameshangazwa na Meneja TANECU kuchukua uamuzi wa makubaliano hayo wkati uamzi wa nini kifanyike kutokana  upotevu huo ulitakiwa kufanywa na Wakala wa Leseni za Maghala.  Kufuatia hali Hiyo Mheshimiwa Byakanwa ameagiza Meneja wa TANECU Mohamed Nassoro pamoja na Mwendesha Ghala, Msafiri Zombe akamatwe na kufikishwa katika vyombo vya dola.

Afisa Ushirika atumbuliwa
Kuhusu usimamizi wa malipo ya wakulima Mheshimiwa Byakanwa ameagiza Afisa ushirika halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba Sudi Said Rajabu akamatwe na kuchukuliwa hatua za kinidhamu kwa kosa la kuruhusu wakulima kulipwa kupitia akaunti binafsi ya Katibu wa chama cha Msingi cha Upendo ndugu Kazumari Mkadimba kinyume na utaratibu. Amesema jumla ya shilingi 1,147,465,168/=  za wakulima zililipwa kupitia akaunti binafsi ya Katibu huyo jambo ambalo linakinznaa na utaratibu wa serikali wa malipo kupitia akaunti ya mkulima husika. sambamba na hilo Mheshimiwa RC ameagiza kufanya uchunguzi iwapo wakuilima wamelipwa stahili zao.


Malipo Hewa
Vilevile Mheshimiwa byakanwa ameagiza kukamatwa kwa viongozi wa vyama vya msingi waliofanya malipo hewa. Ameelea kuwa msimu wa mwaka 2016/2017 vyama 12 vilifanya malipo hewa ambayo thamani yake ni shilingi 117,276,002.00 na hivyo kusababisha wakulima 156 kukosa malipo. Msimu wa mwaka 2017/2018 tume iligundua vyama 28 kufanya malipo hewa ambapo jumla ya shilingi 395,783,836.06 zililipwa na hivyo wakulima 328 kukosa malipo. Licha ya viongozi hao na wanufaika wa malipo hayo kukamatwa ameelekea akaunti zao na zile za vyama vyao vya msingi kushikiliwa kupisha uchunguzi.

Ucheleweshaji wa malipo
Mheshimiwa Byakanwa amesema uchunguzi wa Tume, pia umebaini kuwa baadhi ya vyama vya Msingi vilichelewesha kuwalipa fedha wakulima wa korosho ilihali Chama Kikuu cha Ushirika TANECU kikiwa kimeingiza fedha husika kwenye vyama vya Msingi. Katika msimu 2017/2018 uchunguzi umebaini vyama vya msingi 43 vilichelewesha kuwalipa wakulima 3,343, sawa na  kilo 1,286,163 zenye thamani ya  Tsh. 3,029,488,791.12 hivyo Mheshimiwa Byakanwa ameagiza malipo hayo yafanyike mara moja ndani ya wiki mbili na kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya isimamie suuala hilo.

 Kulipa korosho nje ya Mfumo.
Uchunguzi umebaini katika Msimu 2016/2017 na 2017/2018 vyama vya msingi 20  kupitia viongozi wao wamefanya ubadhirifu na kusababisha kilo 161,869 za Wakulima 624, sawa na, Tsh 277,521,962.26 kutokulipwa malipo yao. Ameagiza viongozi hao kukamatwa na akaunti zao kufungwa na kushtakiwa kutokana na ubadhilifu walioufanya.

Mfumo ulio rasmi katika biashara ya korosho unaanzia pale Mkulima anapopeleka korosho kwenye chama cha msingi na kupewa stakabadhi inayojulikana kama CPR, chama cha msingi kinasafirisha korosho kwenda ghala kuu TANECU kwa ajili ya mnada na kutoa stakabadhi kwa Chama cha msingi inayojulikana kama WHR. Baada ya TANECU kuuza korosho kwa njia ya mnada na kukata makato mbalimbali ikiwemo ushuru wa Halmashauri ndipo fedha zinaingizwa kwenye akaunti ya chama husika. Utaratibu huu haukufuatwa.

Vilevile Mheshimiwa Byakanwa ameagiza benki pia kufanya marekebisho katika utendaji wao kwa kuharakisha malipo ya fedha kwa wakulima. Amesema zipo benki ambazo pia zilichelewesha malipo ikiwemo kuhamisha fedha kutoka benki moja kwenda nyingine.

Byakanwa amehitisha kwa kuahidi kuwa kwa muda wote atakaokuwa Mtwara hataruhusu mianya ya kunyanyasa wakulima. Kwa yeyote atakayebainika kufanya kinyume na utaratibu atachukua hatua za kisheria. Amewataka wananchi wote wa mkoa wa Mtwara kufuata utaratibu katika utendaji kazi na kujiepusha na mambo yatakayowafanya waingie katika migogoro isiyo ya lazima.

No comments:

Post a Comment