MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Saturday 16 December 2017

Walimu wa sekondari Mtwara kuhamishiwa Msingi




Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Mheshimiwa Gelasius Byakanwa amemuagiza Katibu Tawala Mkoa, Alfred Luanda kuangalia uwezekano wa kuwahamisha walimu wa sekondari ili wafundishe shule za Msingi. Mheshimiwa Byakanwa ametoa agizo hilo wakati wa kikao wa wadau wa Elimu mkoani Mtwara kilichofanyika jana kwenyeukumbi wa Chuo cha Ualimu Mtwara Kawaida.
 
Amesema haiwezekani mkoa ukakaa kusubiri Wizara ilete walimu wakati walimu wapo. Kinachotakiwa ni kufuata utaratibu na kuangalia walio na sifa za kufundisha shule za Msingi waende bila kuathili mishara yao.

Ametoa agizo hilo kufuatia taarifa ya Afisa Elimu Mkoa Fatuma Kilimia ambayo ilionesha ziada ya walimu 608 wa masomo ya sanaa kwa shule za sekondari Mkoani hapa wakati shule za Msingi Mkoani hapa zikiwa na upungufu wa Walimu 2,836.
Katika taarifa hiyo Kilimia alieleza kuwa mahitaji ya walimu wa masomo ya sanaa kwa shule za sekondari Mkoani Mtwara ni 1490 waliopo 2098 hivyo kufanya ziada ya walimu 608.

Wakichangia katika kikao hicho kilichokusudia kuangazia changamoto za elimu kwa mkoa wa Mtwara wadau wameitaka serikali kuhakikisha inapambana na masuala mbalimbali yanayozuia maendeleo ya elimu.

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Nanyamba Mheshimiwa Abdalah Chikota ameitaka serikali ihakikishe inafuatilia mwenendo wa elimu kuanzia ngazi ya shule ili kuhakikisha kila mmoja anawajibika kwa nafasi yake na wanaobainika kutotimiza wajibu wao wawajibishwe. Pia ameitaka serikali kuhakikisha mfuko wa elimu kwa kila halmashauri unasimamiwa ili utumike kwa lengo lililokusudiwa.

Aidha Mkuu wa Shule ya sekondari Mitengo Mwalimu Amina Bakari ameitaka serikali iweke viwango ambavyo kila atakayeshindwa kuvifikia atawajibishwa.
Akiridhia wazo hilo Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa ameagiza kila shule kuhakikisha zinakamilisha mtaala wa darasa husika mwezi wa sita wa kila mwaka ili muda unaobaki utumike kufanya majaribio na marudio ya vipengele mbalimbali ndani ya masomo husika. 

Mkoa wa Mtwara umekuwa haufanyi vizuri katika mitihani mbalimbalia ya kitaifa hali ambayo inamfanya Mkuu wa Mkoa Mhe. Byakanwa aliyechaguliwa kuongoza mkoa huu hivi karibuni kuitisha kikao hicho chenye lengo la kutafuta ufumbuzi wa changamoto hizo. Katika matokeo ya darasa la saba mwaka jana mkoa ulishika nafasi ya 22 kati ya mikoa 26.

No comments:

Post a Comment