MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Monday, 20 November 2017





Katibu Tawala Mkoa wa Mtwara Alfred Luanda amewataka Maafisa Utumishi kubuni njia nzuri itakayotoa motisha kwa watumishi ili kuwafanya wawe na moyo wa kufanya kazi ndani ya mkoa. Amesema anatambua ugumu wa mazingira na huduma katika baadhi ya maeneo ndani ya mkoa lakini mipango mizuri yenye kutoa motisha kwa watumishi itawafanya watumishi waendelee kuwa na moyo wa kufanya kazi katika maeneo waliyopangiwa.

Luanda ameyasema hayo leo wakati akifungua Warsha ya kuandaa mipango ya motisha ya watumishi wa serikali za mitaa iliyofanyika katika ukumbi wa Chuo cha Maafisa Tabibu Mtwara (COTC)

Katika warsha hiyo iliyoandaliwa na shirika la Watu wa Marekani (USAID) kupitia mradi wake wa PS3 amesema jambo kubwa ni halmashauri zenyewe kujiangalia ili yale ambayo wanauwezo nayo yapewe kipaumbele katika utekelezaji.


‘Ni kweli kuwa utekelezaji wa baadhi ya mambo unahitaji fedha nyingi mfano, ujenzi wa barabara, ujenzi wa nyumba za watumishi, miundombinu ya mawasiliano na mengine mengi. Haya Serikali itaendelea kuyashughulikia kwa kadiri inavyopata uwezo wa kutekeleza’.

Amesisitiza kuwa utoaji wa motisha kwa watumishi utakuwa na maana tu kama utakuwa endelevu hivyo ni vema mipango ikajengwa ndani ya mifumo ya utendaji wa Halmashauri, ili iwe rasmi, endelevu na kuingizwa katika mifumo ya ufuatiliaji na uwajibikaji.

Kwa upande wake Msimamizi idara ya Rasilimali Watu Kanda ya Kusini, Mradi wa PS3, Restituta Evaristy Masau amesema wazo la motisha kwa watumishi wa serikali za mitaa limekuja kufuatia utafiti uliofanywa na shirika lao wakipitia sera ya motisha kwa wafanyakazi na kubaini kuwa ni ngumu kuitekeleza.


Kufuatia utafiti huo ndipo shirika likaona umuhimu wa kuwapa mafunzo Maafisa wa Halmashauri ili waweze kuandaa mpango unaotekelezeka. Anasema mradi huo wa PS3 unaodhaminiwa na watu wa marekani una nia ya kuhakikisha watanzania wanaondokana na changamoto wanazokutana nazo katika mazingira ya kazi, hivyo kuachana na tabia ya kuhama hama kituo kimoja kwenda kingine kwa kisingizio cha mazingira magumu ya kazi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Warsha, Tamko Mohamed Alli ambaye pia ni Afisa Utumishi Manispaa ya Mtwara Mikindani anasema ziko changamoto nyingi katika halmashauri za mkoa wa Mtwara ambazo zinawafanya watumishi kupenda kufanya kazi eneo moja na kuchukia maeneo mengine. Anasema kubwa linalowavutia ni miundombinu ya eneo husika hivyo warsha hiyo itakayoendeshwa kwa siku tano itasaidia kwa kiasi kikubwa kupata mpango mpya wa motosisha kwa wafanyakazi.


No comments:

Post a Comment