MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Sunday 26 May 2019

Mambo ya kuzingatia kwa mgonjwa wa Kisukari

Na; Herieth Joseph Kipuyo - Afisa Lishe, Evaristy Masuha-Afisa Habari-    Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mtwara
Kwa wasomaji wapya. Hii ni sehemu ya nne ya makala zinazozungumzia Lishe  ya jamii. Wiki iliyopita tulizungumzia namna mgonjwa wa kisukari anavyoweza kula vyakula kutoka katika makundi makuu matano ya vyakula bila kusababisha  wingi wa sukari kwenye damu. Leo tunaendelea kuzungumzia mambo ambayo mgonjwa wa kisukari anashauriwa kuzingatia sambamba na ulaji. Tuwe pamoja.

 Epuka matumizi ya pombe. pombe inatoa nishati lishe kwa  wingi hivyo huweza kusababisha ongezeko la sukari katika damu. (Gm 1 ya pombe ni sawa na kalori 7 hivyo bia moja ni sawa na kalori 840 ambapo ni sawa na mkate mdogo wa silesi).
Pendelea  maziwa yaliyopunguzwa mafuta (low fat milk) usizidishe mililita 250 kwa siku. Kiasi kikubwa cha sukari iliyopo kwenye maziwa ni lactose ambayo haihitaji insulini katika kumeng'enywa. Mgonjwa anashauriwa kutumia maziwa kwa kiasi kidogo kwani ina lehemu (cholesterol)  kwa wingi ambayo huweza kuziba mishipa ya damu na kumsababishia mgonjwa tatizo lingine la magonjwa ya moyo.


Tumia kiasi kidogo cha chumvi. Chumvi inapotumiwa kwa wingi humweka mgonjwa katika hatari ya kupata tatizo lingine la shinikizo kubwa la damu. Matumizi ya chumvi kwa mtu mmoja kwa siku ni gramu 5 (kijiko kidogo cha chai).

Fanya mazoezi ya mwili angalau dakika 30 na kutokwa jasho kila siku. Mazoezi ya mwili husaidia mwili kutumia sukari kwa ufanisi na hivyo kupunguza kiwango cha sukari katika damu.

Epuka msongo wa mawazo

Epuka unene uliozidi. Tafiti zinaonesha kuwa unene uliozidi au kupita kiasi husababisha seli za mwili kushindwa kuitikia mwito wa kichocheo cha insulini kupokea sukari kwa matumizi ya mwili na hivyo kusababisha sukari kuwepo kwa wingi kwenye damu.

Kunywa maji safi na salama ya kutosha angalau glasi nane au lita moja na nusu kwa siku.

 Epuka matumizi ya sigara.
Iwapo unatumia dawa zingatia maelekezo ya dawa uliyopatiwa na mtoa huduma za Afya. Usiache kutumia dawa isipokuwa kwa maelekezo kutoka katika kituo cha kutolea huduma za Afya.

Zingatia maelekezo ya ulaji uliyopewa na mnasihi wa chakula na lishe.

KUMBUKA : Wewe ni nguzo muhimu katika kumudu ugonjwa huu. Tafuta ushauri wa kitaalamu, usikubali kudanganywa na watu wasiokuwa na uelewa mzuri kuhusu ugonjwa huu. Jiunge na kiliniki ya kisukari ili uendelee kuimarisha Afya yako.

Usikose makala ijayo ambayo itajibu maswali mbalimbali  kuhusu ulaji wa baadhi ya vyakula kwa wagonjwa wa kisukari. 

No comments:

Post a Comment