MTWARA RS

FUATILIA TAARIFA MBALIMBALI ZINAZOHUSU MKOA WA MTWARA NA SEHEMU NYINGINE NDANI NA NJE YA TANZANIA, KWA MAWASILIANO E-mail: yustace.evaristy@mtwara.go.tz SIMU: +255 717 697 205

Monday 7 November 2016

Kuelekea Mtwara ya viwanda

 

TANGAZO la Septemba 23, 2016 kwenye gazeti la HabariLeo liliwataka Watanzania hususan wanaMtwara kujitokeza kutoa maoni yao dhidi ya Mpango Kabambe wa Mji wa Mtwara ambao uko katika hatua za mwisho kupitishwa. Jumapili ya Oktoba 10, 2016 Katibu Tawala wa Mkoa huo, Alfred Luanda ambaye pia ana taaluma ya mipangomiji aliwatangazia wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Mtwara siri iliyoko ndani ya mpango huo.

Luanda alisema mpango huo unajibu hoja zote za jinsi mji wa Mtwara utakavyosimamiwa kwa miaka 20 ijayo. Mpango umehusisha eneo lote la Manispaa ya Mtwara Mikindani na kata tisa za Halmashauri ya wilaya ya Mtwara.

Siku hiyo hiyo, kabla ya tangazo la Mpango Kabambe, Kamati ya Ushauri iliridhia ombi la Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, Beatrice Dominic la kuifanya Manispaa hiyo kuwa Jiji. Tafsiri nyepesi ni kuwa wote walioshiriki katika maamuzi haya wana matumaini makubwa na mwenendo wa mkoa katika kukua na kuimarika katika nyanja nyingi za maendeleo.

Kutokana na ukweli kuwa viwanda ni hatua mojawapo ya kuufanya mji kukua, makala haya yanaangazia Mtwara katika azma ya kuelekea mji wa viwanda.

Hali ya sasa viwanda Mtwara.
Ukweli unaoonekana wazi ni kuwa enzi za watumishi kujuta pale wanapopangiwa Mtwara zinaendelea kubaki historia na badala yake sasa watumishi watapigania kupangiwa Mtwara. Mtwara ya sasa ina mvuto mkubwa kwa wawekezaji hasa kutokana na kuonesha uelekeo wa kutatua changamoto ya umeme.

Viwanda vikubwa vilivyopo na ambavyo vinajulikana sana kwa sasa vipo vinane. Viwanda hivyo vitano ni vya kubangua korosho, kimoja cha kuchakata gesi asilia pamoja na viwili vya saruji kikiwemo kiwanda cha Dangote ambacho ni kikubwa kuliko vyote katika Ukanda wa Afrika Mashariki na Kati.

Akizungumza na wamiliki wa nyumba za kulala wageni zilizoko Mtwara mjini mapema mwezi huu, Mkuu wa Mkoa, Halima Dendego aliwahakikishia kuwa mkoa umeweka mazingira mazuri ya kuvutia na kuruhusu uwekezaji na kwamba amekuwa akipokea wageni wengi. Miongoni mwa wageni hao anasema ni pamoja na wale wanaohitaji kuwekeza katika sekta ya viwanda.

Mwanzoni mwa Oktoba mwaka huu viashiria vya Mtwara ya viwanda viliendelea kujionesha baada ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa kukata kiu ya sintofahamu ya muda mrefu ya wakazi wa Mtwara ya kutaka kujua iliko ahadi ya ujenzi wa kiwanda kikubwa cha mbolea cha HELM.

Ntalikwa aliwaeleza wanaMtwara kuwa kiwanda kilichelewa kutokana na hofu ya uwepo wa gesi asilia ya kutosha na kwamba sasa upo uhakika usioacha chembe kwamba rasilimali hiyo ipo ya kutosha kuwezesha kiwanda hicho kujengwa.

Alieleza kuwa mahitaji ya kiwanda hicho ni futi za ujazo trilioni 0.8 wakati vituo vya Ntorya na Msimbati vyote vya Mtwara vina uwezo wa kuzalisha futi za ujazo trilioni 2.05, hivyo ni wazi kuwa kiwanda cha HELM kinakuja katika eneo la MsangaMkuu mkoani hapa.

Kwa nini viwanda havikwepeki mkoani Mtwara?
Mambo makubwa yanayoipeleka Mtwara kuwa eneo la Viwanda ni uwepo wa umeme wa kutosha na wa uhakika unaotokana na ugunduzi wa gesi asilia na mipango ya mapema ya kuupanga Mji wa Mtwara kupitia Mpango Kabambe wa mji huo.


Mengine ni jiografia na historia ya mkoa. Kwa sasa wengi wanaoiangalia Mtwara kwa kuitofautisha na mikoa mingi ya nchi hii ikiwemo Dar es Salaam ni kukamilika kwa wakati kwa Mpango Kabambe wa mji huo. Hii ndiyo njia moja kubwa anayoiamini mwekezaji kuwa itamuepusha na migogoro ya ardhi.

Mpango huu unakuja wakati mkoa haujaingia katika ujenzi holela kama ilivyo mikoa mingine hapa nchini. Mtwara ni mji ambao unafananishwa na mji wa Tanga kwa kupangika sawasawa. Rais mstaafu Jakaya Kikwete alipotembelea mkoa wa Mtwara wakati wa ufunguzi wa Kiwanda cha Dangote na kile cha kuchakata gesi asilia cha Madimba aliusifia mji kwa kuwa na mpangilio mzuri.

Hili limewezekana kutokana na historia ya mkoa kuwa ulipimwa na wakoloni, kisha ukasimama kuendelea kutokana na sababu za kihistoria hasa mapambano ya ukombozi wa nchi za kusini mwa Afrika.

Barabara za Mtwara zimepangika vizuri na pana kiasi kwamba upanuzi wa mji hautahitaji kubomoa nyumba. Hiyo ni ziada ya matumaini ya kuiona Mtwara ya maendeleo ya viwanda ikiendelea kuwa na mwonekano mzuri. Licha ya sifa ya kuwa na Mpango Kabambe wa Mji, mkoa unayo ardhi ya kutosha kwa kilimo na shughuli nyingine za uwekezaji.

Hii imekuwa ikichangia mkoa kuongoza kwa asilimia 75 ya uzalishaji wa korosho nchini Tanzania. Zao hili pia ni mvuto kwa wawekezaji wa viwanda vya kubangua korosho.

Andiko la Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Halima Dendego, ‘Opportunity for Investment’ linalopatikana katika http://www.mtwara.go.tz/pages/the- opportunities-for- investment linaonesha kwamba mkoa wa Mtwara wenye eneo la kilometa za mraba 16,720 unazo hekta 1,400,00 zinazofaa kwa kilimo.

Dendego anafafanua kuwa eneo hilo lina rutuba ya kutosha na halijatumiwa ipasavyo hivyo anaalika wawekezaji kulitumia.

Kwenye barua ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa Mtwara Mikindani kuwashawishi wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa kuifanya Mtwara kuwa jiji anataja baadhi ya mambo ambayo yanaonesha kuwa mkoa huo ni endelevu.

Anasema Mji wa Mtwara ndio kitovu cha uchumi wa mikoa ya kusini mwa Tanzania ikiwemo Lindi na Ruvuma. Mkoa huu kwa sasa unajengwa Tawi la Benki Kuu ambalo kwa mujibu wa Rais mstaafu Kikwete wakati akiwaaga wakazi wa Mtwara, tawi hilo limekuja kutokana na viashiria vya kukua kwa haraka kwa mji huo.

Kikwete ambaye mpango wa ujenzi huo ulianza katika kipindi chake cha uongozi anasema anaiona Mtwara itakayokuja kuwa mhimili wa uchumi wa nchi hii. Ujenzi wa reli itakayosaidia kusafirisha makaa ya mawe toka Liganga na Mchuchuma uko katika hatua nzuri.

Upanuzi wa Bandari ya Mtwara ikiwemo mpya ya Kisiwa Mgao iliyoko katika mipango ya ujenzi ni viashiria vipya vya mvuto kwa uwekezaji wa viwanda.

Barabara nzuri, bandari, reli, na uwanja wa ndege vyote vinapatikana mkoani Mtwara, mambo ambayo yanaonesha kuwa Mtwara ni ya viwanda inawezekana.

No comments:

Post a Comment